Majira ya joto (summer) ndio yanakaribia kuisha. Kwa jiji kama la Toronto mabadiliko hayo ya hali ya hewa yanamaanisha mwanzo wa safari nyingine ndefu kabla ya majira kama haya kurejea tena. Matamasha na mikusanyiko inapungua kwa asilimia kubwa sana kama sio zote.Kanada ni nchi yenye baridi sana.
Mojawapo ya mambo ambayo nimejaribu kufanya mwaka huu katika majira haya ya joto ni kuhudhuria matamasha na mikusanyiko mbalimbali ambayo lengo lake ni kutukuza na kulikumbuka bara la Afrika katika njia nzuri(positive Africa). Nimehudhuria na hata ile isiyokuwa na uafrika ingawa ukweli ni kwamba popote pale ambapo shughuli zimegongana basi upendeleo nimeutoa kwa afrika. Muziki na vyakula vya kiafrika vimekuwa mbele zaidi katika kulitendea mema bara letu. Tumecheza na tumekula vyakula mbalimbali kutoka Afrika. Tumewaalika watu wote,kutoka pande zote za dunia.Nao wamependa vyakula na muziki wetu.Cha ajabu wameupenda kuliko hata sisi wenyewe.
Katika matamasha mengi ambayo nimehudhuria mwaka huu wakati wa majira ya "summer" hakuna ambalo limenivutia kama hili nililohudhuria jana.Linaitwa
FESTIVAL BANA Y'AFRICA . Wanamuziki wengi mahiri kutoka barani Afrika na wale wanaoishi hapa Kanada walipamba vilivyo tamasha hilo.Uzuri wa sehemu lilipofanyikia tamasha hili,vyakula vilivyokuwepo nk. vilitosha kukonga nyoyo za waafrika wengi waliohudhuria.
Yote tisa,kumi na kilichonivutia sana ni kumuona kwa mara ya kwanza mwanamuziki Adam Solomon (pichani juu akicharaza gitaa) baada ya kusikia sifa zake nyingi kupitia mashabiki,vyombo vya habari kama tv na redio. Baada ya kumshuhudia akifanya vitu vyake jukwaani nilipata bahati ya kuhojiana naye machache kuhusiana na kazi yake na mafanikio ambayo ameyapata. Alinieleza mengi ambayo bado nayafanyia kazi na yakikamilika nitayarusha hewani.
Adam Solomon ni mzaliwa wa Mombasa,Kenya ambaye hivi sasa anaishi na kuendesha kazi zake za mziki hapa Kanada akiwa na kundi lake zima la bendi ya Tikisa.Zaidi wanajulikana kama Adam Solomon and the Tikisa Band. Adam anaimba nyimbo zake nyingi katika lugha ya kiswahili jambo ambalo linavutia sana. Alitusisimua sana alipocheza kibao cha zamani cha Less Wanyika cha "Sina Makosa". Less Wanyika ni mojawapo ya bendi maarufu zilizowahi kutokea barani Afrika na Adam aliwahi kuwa mmojawapo wa wanamuziki wa kutegemewa wa bendi hiyo.Adam ni mahiri sana katika kupiga gitaa na hivi karibuni alifanikiwa kutwaa Juno Music Award. Hii tunaweza kusema ndio Grammy Awards ya Canada. Unaweza kusikiliza baadhi ya vibao vyake
hapa na pia
hapa. Hizi ni albamu zake mbili ambazo ameshazitoa. Furahia maisha yako na muziki wa Afrika.
Asante kwa habari hii kuhusu Adam na muziki wake.