Sina hili wa lile,nimejipumzisha nikijaribu kuwa baba bora.Maisha ya ughaibuni yanataka moyo jamani.Waliopo huku watanisaidia kwa hoja hii.Simu inaita,ni Boniface Makene kutoka Texas,Marekani. Ananipa habari ambazo kwa kweli sio njema na hazipendezi kabisa katika karne hii ya ahadi ya usawa na uwazi,uhuru wa habari,uhuru wa kujisomea na kuchambua masuala mbalimbali.Gazeti ambalo naliandikia makala kila jumapili la Tanzania Daima limefungiwa kwa siku tatu.Kisa na mkasa kisome hapa.
Sheria iliyotumika ni sheria ya magazeti namba 3 ya mwaka 1976!Hili kwanza linanitia simanzi.Hivi kweli leo hii ukizingatia jinsi dunia ilivyobadilika ni halali kutumia sheria ya mwaka 1976?
Nadhani wakati umefika wa nchi yetu kukubali kubadilika na pia kuangalia masuala ya msingi zaidi. Huku ughaibuni kila siku jioni watu hukaa mbele ya luninga zao na kuangalia jinsi ambavyo viongozi wao hufanyiwa kebehi na watangazaji na wachekeshaji wa tv.Mfano mzuri ni bwana huyu anayeitwa Jon Stewart.Wapo wengine wengi tu. Ukitembelea tovuti yake unaweza pia kutazama baadhi ya dhihaka ninazozizungumzia. Sasa najaribu kujenga picha,raisi Bush angekuwa anapambana na watu kama hawa ingekuwaje?Je hii ina maanisha kwamba hatuna mengine ya msingi ya kuyafanyia kazi?
Ni kweli kwamba tamaduni zetu sio sawa na za Marekani,Canada au kwingineko.Lakini je leo hii tunaweza kusimama pembeni tukasema tuna tamaduni zetu?Tukasema kwamba raisi wetu hawezi kutaniwa? Je,habari hii kama ililengwa kwenye kumdhalilisha raisi wetu, ilisomwa na watu wengi zaidi hiyo Novemba 6 au sasa ambapo dunia nzima inatuangalia? Busara imetumika kweli hapa? Ngoja niishie hapa kwa leo!Sidhani kama kwa hali hii nitaeleweka hata nikiandika mpaka asubuhi.
Safari ya mashua yetu inazidi kusongwa na mawimbi. Namtazama jemedari wetu kasimama akihamaki katika kilindi. Siku zapaswa kwenda na lazima tufike, machafuko haya yanaleta upepo mkali kutazama lakini nasikia waelekeza manyunyu katika sehemu kame. Tabu yetu sisi baharini kumbe yaweza kuwa liwazo kwa watu alfu nyingi. Sioni shaka kama hili ndilo lengo la upepo huu, bora uje na hata upasue mashua hii kabisa! Lakini nani atafaidika na mvua inayotokana na upepo huu kama wakulima wa nchi hii hawana zana bora za kilimo, hawana mbegu baada ya zile walizobakiza kuzigeuza chakula wakati ule wa kiangazi! Hapa ndipo ninapopigana na moyo wangu juu ya maamuzi yapi thabiti kusimamia.
Maoni yangu yataka utulivu Jeff, fikiri na tazama shida hizi za mashua hii tuliyopanda mimi na wewe na faida ya upepo ambao unatangaza kilio cha maisha yetu!