VIJIMAMBOZ PROUD AFRICAN KASRI LA MWANAZUO BONGOCELEBRITY NKYA MAWAZO NA MAWAIDHA JIKOMBOE MIRUKO NDABULI SHAMIM ZEZE DAMIJA MATERU MLOYI CHEMI CHE MPONDA BAKANJA MTAFITI LUKWARO MSANGI MDOGO MARK MSAKI DIRA YANGU MWAIPOPO KONA YANGU FURAHIA MAISHA YAKO DAMIJA MICHUZI FATHER KIDEVU MWANDANI NGURUMO FATMA KARAMA ZAINAB OMEGA NGOLE YAHYA CHARAHANI JARIDA LA UGHAIBUNI NYEMBO BWAYA BHALEZEE JUNGU KUU WATOTO WETU BLG BROTHER SAA YA UKOMBOZI NURU AKILINI TAFAKARI ZA MAISHA ALBERT WILSON UCHUMI MIDRAJI IBRAHIM Lucassano CHESI HAKI NGOWI KISIWA CHA AMANI Innocent Kahwa SULTAN TAMBA SIMON KITURURU MAVIZO MUSA NGARANGO KIJIWENI(NED) WATANZANIA JADOUNG METTY MAGGID MJENGWA SAHARAN VIBE MWENYE MACHO ABDALLAH MRISHO MYAFRICA SHERIA NA MAVAZI
NEW VISION UGANDA MONITOR UGANDA KENYAN NATION MEDIA EASTANDARD FROM AFRICA BUSINESS WEEK ALL AFRICA
MAGAZETI YA IPP UHURU NA MZALENDO BUSINESS TIMES DAILY NEWS TANZANIA DAIMA MWANANCHI BUNGE LA TANZANIA SERIKALI YA TANZANIA IPS INTERNATIONAL
AFRIKA HURU NINI KILITOKEA PAMBAZUKA DUNIA YETU GADO CARTOONS
SEND ME AN E-MAIL
Friday, January 05, 2007
MATEMBEZI KATIKA JIJI LA KARNE!


Naomba nianze kwa kukutakia kheri ya mwaka mpya. Kwa takribani wiki tatu nilijaribu kukaa mbali na mtandao ili kupumzisha akili,kutafakari yaliyojiri mwaka tulioupa kisogo hivi majuzi na kupanga mikakati mipya ya 2007 kama ikibidi. Tofauti na miaka iliyopita, mwaka huu sijaweka malengo maalumu.Nataka uwe mwaka shaghalabaghala kama itawezekana.Wewe unasemaje? Lakini jambo moja ambalo nipende nisipende tayari lipo kwenye malengo
na ajenda za mwaka huu ni suala la
kuendelea kublog.


Wakati wa kufunga mwaka nilitembelea kwa Joji Kichaka kama ambavyo Ndesanjo hupenda kumuita. Katika pita pita zangu nilitembelea mojawapo ya ile "miji shoka" ambayo mingi imegeuka kuwa namna ilivyo baada ya kuhamwa na watu weupe. Historia ndio inayosema hivyo,sio mimi.Kuhamwa huko kulipewa jina "white flight" ikimaanisha wazungu kuhama na kuwaacha weusi waendelee kukaa wenyewe katika miji yao.Kilichochangia sana ni ubaguzi wa rangi ambao mpaka hivi leo ungali upo na pengine utaendelea kuwepo milele.Wachumi wanasema sababu za kiuchumi ndio zilizochangia "white flight".


Jiji la
Gary(mpaka hivi sasa sielewi nini kinasababisha sehemu moja kuitwa jiji na nyingine kuitwa mji au kijiji) lipo katika jimbo la Indiana mpakani kabisa na jimbo la Illinois lenye jiji maarufu la Chicago ambapo mwanamama Oprah Winfrey huendesha shughuli zake. Nia yangu ya kutembelea Gary,Indiana ilikuwa kuanzisha kasumba ya kutembelea kule wanakoishi "wenzetu" na kuachana na kasumba ya kutembelea majiji makubwa peke yake( yale ambayo wenyewe hupenda kuyaonyesha kwenye sinema zao na kurubuni wengi duniani kwamba Marekani ndivyo inavyomeremeta).Pia nilitaka kuona mahali mwanamuziki maarufu wa muziki wa pop Michael Jackson na ndugu zake kina Janet Jackson,Tito Jackson,LaToya Jackson, Marlon Jackson,Randy Jackson,Jackie Jackson na Rebbie Jackson walizaliwa na kuanzia maisha yao ya uanamuziki.

Pichani juu ni nyumba walimozaliwa nyota hao wa muziki ambapo baadaye kaka yao Michael Jackson alikuja kuwa na umaarufu wa aina yake wenye mchanganyiko wa mambo chungu tele. Tofauti na nyumba zingine zilizopo katika jiji la Gary nyumba walimozaliwa nyota hao wa muziki inaonekana kuwa safi,inayotunzwa na ina hata majani ya kupandikiza. Sababu ni kwamba familia ya wanamuziki hao imeamua kuitunza nyumba hiyo kwa ajili ya kumbukumbu (souvenir ) kama ilivyokuwa enzi hizo.Hivi sasa kuna mpangaji anayeishi humo.Nyumba hiyo iko katika kijimtaa kidogo ambacho kwa heshima ya familia ya Jacksons nacho kinaitwa Jackson Street. Mwaka uliopita(2006) jiji la Gary lilitimiza miaka 100 na hivyo kuchukua jina la jiji la karne!


Jambo ambalo litakushtua ukifika Gary,Indiana ni hali ya maisha,uchakavu wa majengo,vichaka,uchafu na kila aina ya takataka za dunia hii. Picha ya pili hapo juu ni mfano wa nyumba nyingi nilizoziona. Nyumba hiyo ni makazi ya mtu ndani ya Marekani.Ilikuwa vigumu kwangu kuamini kwamba hii ndio Marekani ambayo inatumia mabilioni ya dola kupigana vita inavyojua kabisa kwamba kamwe haitaweza kuvimaliza bila kurekebisha sera muhimu za ndani na nje.Hii ndio nchi ambayo viongozi wake wanajifanya hawaoni umasikini na uharamia unaojiri nyumbani na hivyo kuyafumbia kabisa macho masuala hayo.Nilichokiona mimi ni kama uwanja wa vita au jamii ambayo imehamwa baada ya mapigano ya muda mrefu. Hapana,nilikuwa nimekosea; hapo ni Gary,Indiana jiji lenye wakazi zaidi ya laki moja na nusu. Damu ilikuwa inasisimka huku vinyweleo vikisimama kila mara.Au ni uoga wangu tu?


Kama nilivyoeleza hapo juu,jiji la Gary ni mojawapo ya majiji mengi ya Marekani ambayo yalikumbwa na "white flight", mengine ni kama vile Philadelphia, Atlanta, Houston, Miami, Cleveland, Boston, Detroit, Memphis, St.Loius, Milwaukee, New Orleans(Katrina), Magharibi na Kusini mwa jiji la Chicago, maeneo kama Bronx, Oueens(Coming to America), Brooklyn na kwingineko. Kitakwimu (wakati mwingine sipendi kuziamini) miji kama hiyo niliyoitaja hapo juu inaongoza kwa kuwa na ghasia,mauaji na gharika chungu mbovu za kijamii. Kwanini ni swali gumu kujiuliza lakini muhimu. Hivi sisi weusi hatuwezi bila wazungu? Nini kilitokea katika historia ya binadamu,historia yetu? Kuna mkono wa mtu?


Mwishoni swali la kwamba kwanini Marekani haisaidii wananchi wake kama hawa wa Gary,Indiana jiji ambalo kila mara limo kwenye orodha ya miji hatari kupita yote nchini Marekani, inahangaika kuihadaa dunia kwamba inapeleka maendeleo na demokrasia duniani? Hivi ni kweli kwamba zipo Marekani mbili tofauti kabisa ndani ya Marekani tunayoijua sisi?Tuendelee kublog,2007 ndio hiyo.
 
Muandishi: Jeff Msangi |Tarehe: 2:46 PM | Permalink |


Maoni: 15


  • Tarehe: 4:44:00 PM, Mtoa Maoni:- Anonymous Anonymous

    Jeff, msikilize John Edwards (aliyekuwa mgombea mwenza wa Kerry uchaguzi uliopita) ambaye ametangaza kugombea urais. John Edwards (ambaye yeye na mke wake ni wanablogu) amekuja safari hii na ujumbe mmoja mzito: Marekani mbili. Ulichozungumzia hapa ndicho anachoongelea huyu bwana. Anasema ndio ugonjwa mkuu wa Marekani. Nchi hii ni sawa na nchi mbili. Nchi ya wachache ambao maisha yao yanadhaniwa kuwa yanawakilisha maisha ya Wamarekani wote. Na wamarekani wengi ambao, ingawa unaweza kuona wana magari na wanaishi ndani ya nyumba, wanaandamwa na madeni hadi mvunguni. Jamaa mmoja aliyekuwa jirani yangu hivi sasa kawa ombaomba. Aliachishwa kazi, akawa anaumwa, mwenye nyumba hakusikia kitu anachotaka ni fedha yake. Akamletea polisi, huyo akatolewa nje. Sasa anaombaomba huku akitafuta kazi!

    Ndio ulichosema hapo. Kuna nchi mbili Marekani. Pengine tatu. Ndio mabilioni hayo yanatumika "kueneza demokrasia" (demokrasia ya kuua kwa kamba ya katani kama vile tunaishi karne ya kwanza) kule Iraki.

    Mkongo mmoja rafiki yangu alikuwa akisema Marekani ni sawa na barabara ya lami. Unapoendesha gari kwenye barabara ya lami wakati wa jua kali unaona kama barabarani mbele yako kuna maji. Ukifika hapo panapoonekana kama pana maji unakuta hakuna kitu. Kwa lugha yao wanaita "mirage." Ndio Marekani hiyo yenye Gary, Indiana na miji mingine ambayo wanaishi akina Cheney na wezi wenzake na vibosile vya makampuni makubwa yanayohonga wawakilishi hapa ili kusipitishwe sheria ya kima cha chini.

     
  • Tarehe: 4:54:00 PM, Mtoa Maoni:- Blogger Simon Kitururu

    Duh !Kazi ipo!

     
  • Tarehe: 6:57:00 PM, Mtoa Maoni:- Blogger Egidio Ndabagoye

    Mm!na hii ni Marekani? kumbe ni tofauti sana na zile picha za Hollywood.

     
  • Tarehe: 2:07:00 AM, Mtoa Maoni:- Blogger mwandani

    American dream! - ahsante kwa kutuhabarisha.

     
  • Tarehe: 4:31:00 PM, Mtoa Maoni:- Anonymous Anonymous

    Karibu tena, nilikuwa najiuliza huyu bwana kazamia wapi? Hongera na mwaka mpya.

     
  • Tarehe: 5:17:00 PM, Mtoa Maoni:- Blogger MICHUZI BLOG

    Jeff!

    Karibu tena ulingoni. Natumai umemsoma Ndesanjo kwa makini. Hakika yake ni mwangwi wa nilotaka kunena. Aisee umekuwa mvivu siku hizi. Bize nini?

     
  • Tarehe: 9:37:00 AM, Mtoa Maoni:- Blogger Jeff Msangi

    Michuzi,
    Nimerejea kaka usiwe na shaka.Nilibanwa na majukumu ya hapa na pale na pia likizo kidogo ambayo matunda yake ndio kama hayo hapo juu.

     
  • Tarehe: 9:30:00 PM, Mtoa Maoni:- Blogger Mjengwa

    Jeff,
    Asante sana!
    Nami nimesoma maelezo ya Ndesanjo. Hakika ya huko Marekani yamejitokeza hata hapa nyumbani. Tuna Tanzania mbili pia!
    /maggid

     
  • Tarehe: 9:09:00 AM, Mtoa Maoni:- Anonymous Anonymous

    Tanzania mbili, umenena sawa Maggid. Natoa changamoto kwa Michuzi, ningependa atuwekee mfululizo wa picha zinazoonyesha Tanzania hizi mbili. Nawe Maggid pia una kamera yako, tuanzishieni mjadala kwa picha za Tanzania mbili. Jeff unajua angeweza kutuwekea picha za majengo marefu ya vioo na magari ya kifahari n.k. lakini akaamua kutuonyesha jambo lisiloongelewa sana: mafukara wa MArekani.

     
  • Tarehe: 1:35:00 PM, Mtoa Maoni:- Blogger Jeff Msangi

    Ndesanjo,
    Naunga mkono changamoto uliyoitoa kwa Michuzi na Maggid.Kwa namna fulani Maggid amekuwa akifanya hivyo.Tunaomba muendelezo.

     
  • Tarehe: 3:27:00 AM, Mtoa Maoni:- Blogger Patrick G. Kamera

    Jeff,

    Kumbe una blog ya Kiswahili pia!

    Duh! Poa sana ndio naicheki hapa, safi sana.

    Kuhusu Marekani mbili hilo ni kweli kabisa kama ulivyojionea mwenyewe, kuna Wamarekani wanapigika vibaya ila hilo halitangazwi wala kuonyeshwa CNN, ila kuna kipindi cha "Feed the Children" siku nyingine wanaonyesha Marekani fulani hoi bin taabani tofauti kabisa na ile ya Hollywood inayouzwa duniani.

    Tanzania pia tunaelekea hukohuko kama hatujafika, maana wenye navyo wanaendelea kuneemeka na wasionavyo rhumba linazidi kukolea. Tulikuwa nyumbani hivi karibuni tumejionea wenyewe.

    Maswali yanakuja, tumejikutaje katika hali hiyo? Nini kifanyike kama kuna cha kufanya au ndio hivyo tena kila mtu kivyakevyake, mwenye nguvu mpishe, au...

     
  • Tarehe: 9:59:00 AM, Mtoa Maoni:- Blogger Jeff Msangi

    Patrick,
    Ahsante kwa kunitembelea hapa kwenye kiswahili pia.Kimsingi hii ndio blog yangu kuu,nakesha zaidi hapa kuliko hata kule kwenye kiingereza.

    Mwanablog mwenzetu wa blog ya picha anayeitwa Maggid yeye anasema tayari zipo Tanzania mbili au hata tatu.Inasikitisha kuona kwamba tumeshafika huko na hakuna la maana linalofanyika ili kukomesha hali hiyo.

    Patrick,tungefurahi kama ungetupa kidogo tathmini yako kuhusu ulichokiona Tanzania ulivyokwenda hivi karibuni.

     
  • Tarehe: 12:27:00 AM, Mtoa Maoni:- Blogger Patrick G. Kamera

    Jeff,

    Tanzania ziko mbili, si ajabu tatu kama alivyogusia Maggid.

    Maendeleo kulingana na wengi yapo kwenye miji mikubwa ukianzia na Dar. Majengo kadhaa mapya, marefu, ya vioo na mahoteli mapya pia. Nyumba kubwakubwa, nzurinzuri na mageti ya kufungua kwa "remote", zenye walinzi wenye sare maalum na mitambo ya kulindia kama kamera na ving'ora na mikwara kadhaa. Maeneo ambayo ukipita mwenyewe unatia akili!

    Maendeleo mengine ni kwa upande wa magari, yaani ni mengi sana ukilinganisha na wingi(sijui ni uchache) wa barabara zilizopo, hivyo foleni na misongamano ni ya kufa mtu, ni afadhali utembee utawahi unakokwenda.

    Hili limechangiwa niliambiwa na maendeleo "kama ulaya tu" ambapo wafanyakazi kuweza kupata kitu kinachoitwa "soft loans" kuweza kununua magari mradi wana mshahara wa kiwango fulani, hivyo wengi wameichangamkia hiyo mikopo. Matokeo yake kila mtu ana gari pa kuendeshea hakuna, na bei ya petroli iko juu kuliko huku, lakini Wabongo wabishi sijaona, watu wanaburuza madude ya nguvu...

    Vilevile kuna maduka makubwa yanayoitwa "supermarkets" kadhaa na Malls pia zipo. Hizo ni sehemu ambapo wachache wenye ahueni kiuchumi huonekana wakijivinjari humo. Kingine matumizi ya dola ya marekani wakati tuna shilingi yetu, kwenye masuala mengi tu unasikia hii ni dola kadhaa, hii dola kadhaa, ila ukilipia unalipa kwa shilingi lakini kwa kiwango cha dola cha siku hiyo utakachopewa hapo. Hii ni kuanzia kwenye kadi za simu.

    Kila upande kuna mabango na matangazo makubwa ya biashara za simu, sigara na pombe, mabango yenye picha za Rais Kikwete pia yapo hapa na pale(sijui ni mabaki ya kampeni au ndio miondoko ya ki-Kim Il Sung hiyo!)

    Hayo ndiyo baadhi ya maendeleo niliyoyaona Dar-es-Salaam.

    Upande mwingine wa Dar hiyohiyo ambapo ndipo wananchi walio wengi wanapoishi hali ni tofauti kabisa, hilo rumba lake si la kitoto. Nafikiri unaelewa. Huko maji ya kununua kwa ndoo daima, kutoka bombani imekuwa historia ya hapo zamani za kale...kwa hakika karibu nchi nzima nadhani suala la maji kutoka bombani ni ndoto, umeme ndio wala usiseme, ila nasikia baada ya hizi mvua za juzijuzi mgao hakuna tena. Kwa wananch walio wengi umeme wala sio issue, maana wengi hawanao, ni mwendo wa vibatari, mishumaa, kama una jeuri karabai.
    Kijijini nako hakuna nafuu, rumba liko palepale, na cha kutisha zaidi ni idadi ya watu wanaorudishwa au kurudi wenyewe kijijini mwao wakiwa katika hatua za mwisho za kuugua baada ya kuathirika. Hivyo misiba na mazishi imekuwa mingi mno kijijini hadi watu wanashindwa kuacha shughuli zao na kuja kuomboleza pamoja na wafiwa maana utaenda kwa nani utamwacha nani, yaani misiba inaelekea kuwa kama ya huku, familia za wafiwa na ndugu au rafiki wa karibu ambao wanalazimika kuja.

    Na hii yote ni maendeleo!

    Naona niishie hapo, nikikumbuka mengine nitaendelea kukuhabarisha.

     
  • Tarehe: 10:04:00 AM, Mtoa Maoni:- Blogger Jeff Msangi

    Patrick,
    Ahsante sana kwa kipande hiki.Hii ni hali halisi ambayo najua sote tungependa kuona ikibadilika ili maisha yasonge mbele na yanusuriwe pia.Ukiweza endelea kutupa ulichokiona.Shukrani sana.

     
  • Tarehe: 6:03:00 PM, Mtoa Maoni:- Anonymous Anonymous

    Unajua Jeff nilipofika kwa Joji Kichaka nilitazama huku na kule nikaanza kujiuliza, "hivi wale watu weusi tuliokuwa tukiwaona kwenye gazeti la Ebony wako wapi?" Enzi zile nilidhani kuwa watu weusi wote ndio wanavyoishi kama picha za Ebony zinavyoonyesha. Kumbe masahibu ya weusi na weupe pia walio wengi hayaonyeshwi kwenye vyombo vya habari.

    Jambo moja nililojifunza ni kuwa majumba makubwa ya vioo na magari ya kifahari, majumba ya kisasa ya muziki, redio, na luninga ni vipimo hadaa vya maendeleo. Ukipima maendeleo kwa kutazama vigezo hivyo, tuseme kwa Tanzania, utakuwa umedanganyika na pia kutowatendea haki wale wanaoishi bila huduma za afya, maji safi, shule zenye walimu na vifaa, barabara zinazopitika, miji misafi, wakulima wanaotegemea mvua za masika, vijiji visivyo na vituo vya afya, wapiga kura wanaodanganywa, n.k.

    Marekani ndio hivyo nayo. Mfumo wa ubepari ukitumia nguvu ya vyombo vya habari na utamaduni maarufu vimetufanya tukashindwa kujua nini hasa maana ya maendeleo ya mwanadamu.

     
   
 
Copyright 2006 © JEFF MSANGI. All Rights Reserved
 
Idadi ya watu Idadi ya watu Idadi ya watu
eXTReMe Tracker