Raia wa nchi fulani kwa kiingereza anaitwa citizen. Jambo ambalo pengine hujalisikia bado ni “uraia wa kwenye mtandao” au netizen kama ambavyo tunajulikana. Netizen ni uraia wa aina yake kwa sababu ni wa kimataifa, hauna mipaka.
Hati au mkataba maalumu wa netizenship unawataka raia wake kufanya yafuatayo:
1)Kwa kujitolea, kuiendeleza dunia ya mtandaoni kwa iendelee kuwa sehemu ya wazi na yenye mantiki kwa kila mmoja kujivunia na kufurahia.
2)Kuheshimu na kuzilinda haki za binadamu na faragha ya watu wengine na kuziheshimu kama vile ni za kwako binafsi.
3)Kuheshimu kazi za wengine na hivyo kutovuruga uhuru kamili wa habari.
4)Kuzilinda habari binafsi za watu wengine kama unavyolinda za kwako.
5)Kutotumia lugha chafu na zisizopendeza.
6)Kutokutengeneza au kusambaza habari zisizo sahihi.
7)Kutojihusisha na biashara haramu za mitandaoni.
8) Kutotumia majina ya uongo.
Hayo ni baadhi tu ya majukumu ya uraia mwema wa mtandaoni. Nadhani jumuia yetu ya wanablogu wa Tanzania ambao hivi sasa kampeni ya kutafuta viongozi wake zimeshaanza, inaweza ikazitumia baadhi ya kanuni hizo za uraia mwema wa mtandaoni katika kuandika katiba ya kutuongoza.
Chanzo cha mikataba ya kibinadamu kama hii imesukumwa zaidi na ukweli kwamba mtandao unachangia sana kuharibu maisha ya watoto.Wapo watu wazima chungu mbovu ambao kazi yao ni kutafuta watoto wadogo mitandaoni,kuwarubuni,kuwafanya kitu mbaya na hata kuwaua.Inawezekana kirahisi kwani mtandaoni mtu anaweza kujiandikisha kwa kudanganya kila kitu.Babu wa miaka 90 anaweza kujiandikisha kama mtoto wa miaka 10 nk. Nchi zinazoendelea kama Tanzania yetu ni lazima nazo ziamke mapema inavyowezekana katika kuwalinda watoto wa nchi. Tembelea tovuti ya cybertipline uone jinsi wenzetu wanavyojitahidi.
Ahsante sana Jeff kwa taarifa hii.